MAPENZI YA FACEBOOK 08 Nilimtazama mke wangu ambaye kwa wakati huo alionekana kuwa na wasiwasi mkubwa sana, hakuweza kujibu lolote, alizidi kulia huku akinisihi nimsamehe. “Nisamehe bure mume wangu sirudii tena,” aliniambia. “Sitaki kusikia sentensi hii moja kila wakati kwanini lakini umeamua kunifanyia hivi?” “Sio akili yangu ni ibilisi alinipitia?” “Ibilisi?” “Mume wangu niamini kweli sirudii tena.” “Osmon ni nani yako?” “Alikuwa rafiki yangu wa facebook.” “Halafu.” “Ila mume wangu alikuwa akinisumbua sana kila siku alikuwa akinitongoza, kiukweli ilikuwa ni usumbufu ikabidi nimkubalie japo sijawahi kukutana naye wala kufanya naye chochote,” aliniambia Ester maneno yalizidi kuumiza moyo wangu mithili ya kisu butu anachochinjiwa kuku. “Anaishi wapi?” “Yupo Mwanza,” alinijibu jibu ambalo lilinishangaza sana, nilijaribu kuulinganisha ule umbali kutokea Daresalaam mpaka Mwanza lakini sikutaka kuamini kabisa. Yani mtu unakubali kuanzisha mahusiano na mtu ambaye hata hukuwahi kuonana nae mmekutana Facebook halafu unakubali awe mpenzi wako wakati huohuo ni mke wa mtu. Hilo lilizidi kunishangaza sana. Kuna kipindi nilihisi wenda nilikuwa katika jumba la sanaa ya maigizo ambapo nilikuwa nikishuhudia visa na mikasa iliyokuwa ikiendelea katika jumba hilo jambo ambalo lilikuwa si kweli, mke wangu alikuwa akivifanya vitu hivi kwa akili zake timamu. “Kwahiyo ni mpenzi wako?” nilimuuliza. “Hapana,” alinijibu kwa kukataa jibu ambalo lilinishangaza tena. “Wewe siumeniambia huyu ni mpenzi wako halafu unakataa tena?” “Laki…” kabla hajamaliza kunijibu ghafla! Simu yake ikaita, nilipoitazama katika kioo chake ilikuwa ni namba ngeni. Sikutaka kupoteza muda nikapokea. “Ester tangu juzi hupokei simu yangu ni nini kimetokea au kuna kosa nimekufanyia basi nisamehe mpenzi wangu,” ilisikika sauti ikisema kwa kulalamika kwa upande wa pili, kwa kweli sikutaka kuamini kabisa masikio yangu kwa kile nilichokuwa nakisikia. Nilipomtazama Mke wangu bado alionekana kuwa katika wasiwasi sana, machozi yalizidi kumdondoka tu. Sikutaka kujibu jibu lolote lile, nilichoamua kukifanya ni kuikata simu kwa wakati ule. Sijui ni nini kilitokea ila ninachokumbuka nilijikuta nikishikwa na hasira kisha nikaipigiza simu ukutani, ikapasuka vipande vipande. “Ester! Ester! Ester mke wangu,” nilimuita kwa sauti iliyochanganyika na hasira. “Abee mume wangu,” aliitika huku akitetemeka. “Ni nini hiki unafanya, unakosa nini kwangu, ni nini ambacho sikupi mpaka unahadaika na hawa wanaume?” nilimuuliza huku nikivikunja viganja vyangu, nilikuwa katika hasira isiyokuwa na kifani. Wazo la haraka lililonijia kichwani mwangu ni kumpiga mke wangu kiasi cha kumvunja moja ya kiungo muhimu katika mwili wake, wazo hilo nililipitisha lakini lilipokuja suala la utekelezaji nilisita, moyo wangu haukutaka kufanya hivyo. Machozi ya Ester aliyokuwa akiyadondosha huku akizidi kuniomba msamaha sikutaka kuyajali kabisa kwa wakati ule, ni hapa ambapo niliamini katika ule usemi usemao umdhaniaye ndiye kumbe siye. Kwa kweli nilimuamini sana mke wangu, ni mwanamke ambaye aliichukua sehemu kubwa sana katika maisha yangu. Nilimfanya kuwa kama malkia wa ngome ya mapenzi yangu aliyoitawala kiasi kwamba sikutaka kabisa kuchanganya falme. Maisha bila furaha yalikuwa si chochote, furaha hiyo alikuwa nayo Ester, kila kitu alichokuwa akikifanya katika maisha yangu kilizidi kunipa furaha ambayo ilizidi kuyaweka maisha yangu katika usalama wa hali ya juu. “Kama ni kupenda nilikupenda sana mke wangu ila katika hili inabidi nikubali kupoteza kimoja katika maisha yangu ili nibaki na amani ya moyo,” nilimwambia huku nikimtazama. “Tafadhali mume wangu usiniache,” aliniambia huku akiwa amepiga magoti. Nakumbuka ndoa yangu mpaka kufikia wakati ule ilikuwa imetimiza mwaka mmoja, mwaka ambao sikubahatika kupata mtoto kabisa. Kwa kweli sikutaka kuendelea kuishi katika ndoa iliyokuwa ikininyima furaha. Japo nilikuwa nikimpenda sana mke wangu ila ni kama vile kulikuwa na sauti iliyokuja nafsini na kuniambia kuwa sitakiwa kuendelea kuishi katika ndoa iliyokuwa ikinitesa angali bado nilikuwa kijana. “Naomba huu ndiyo uwe mwisho wetu chukua kila kilichokuwa chako uondoke zako, sikutaki tena katika maisha yangu,” nilimuambia maneno yaliyoniumiza kwa kiasi fulani lakini niliamua kujikaza kiume. Je, nini kitaendelea? #Share Kwa wingi.

at 12:45 PM

Bagikan ke

Lintaskan

0 comments:

Copyright © 2025 Braytonofficiallove
Designed by Siyamdezign | Edited By braytonofficiallove
braytonofficiallove | braytonofficiallove | braytonofficiallove
Powered By Blogger
Back to Top