KURUDI KWA MOZA: 28 Walivyofika walishangaa kuona watu wengi sana wamejaa kwa mganga Yule na walipoulizia kwa umakini zaidi, walipewa taarafa ya kuwashangaza sana, “Eti kuna nini?” “Kwani huna taarifa?” “Taarifa gani?” “Mganga amekufa” “Kheee amekufa? Lini tena jamani wakati jana nilikuwa nae” “Ulikuwa nae wapi na muda gani wakati kafa usiku wa kuamkia jana!” Rose alimuangalia mwanae Ana akiwa anashangaa sana. Alishindwa kujibu kuwa alikuwa nae muda gani na wapi kwani kila akikumbuka matukio ambayo kafanya na huyo mganga halafu anaambiwa kuwa amekufa alihisi kuchanganyikiwa kabisa, Yule mwanamke akamuuliza tena, “Ulikuwa nae kivipi ndugu wakati amekufa jana alfajiri na amezikwa jioni” “Kheeee na kuzika tayari?” “Ndio, ila bado nakushangaa ulikuwa nae wapi” “Ni juzi, nimechanganya siku. Yani kifo kimenichanganya hiko” Ilibidi ajigeleshe lakini ukweli ni kuwa kifo cha huyu mganga kilimchanganya vilivyo ukizingatia na yaliyotokea baina yake na mganga huyo siku ya jana, kumbe mganga alikuwa ameshakufa na jioni aliyomuaga ndio alikuwa anazikwa kwakweli Rose alijihisi kudata kabisa. Akaamua asogee kwa mke wa mganga ili apate tetesi kuwa hata ilikuwaje maana bado alikuwa gizani. Alimkuta mke wa mganga akiwa kajiinamia kwa majonzi, na kumpa pole pale kisha kumuuliza kuwa imekuwaje, “Eti imekuwaje tena maana ni gafla sana” “Kweli ni gafla sana, kazi aliyokuwa anafanya mume wangu ni kazi ya hatari sana yani nilijua tu ipo siku nitamkosa kama leo jamani” Huyu mama aliinama tena akilia, basi Rose akawa anambembelea huku akiendelea kumsikiliza kuwa ni kitu gani kilitokea, “Mume wangu aliniambia amepata kazi ya hatari sana, nilimwambia aachane na kazi hiyo ya hatari ila hakunisikia alisema lazima ataifanya. Sasa juzi jioni aliniambia kuwa mteja wake huyo mwenye kazi ya hatari kamzuia asifanye sherehe yoyote maana akifanya hivyo atadhurika yeye kwani nyumba ya huyo mteja alianza kuizungushia dawa huku huku. Usiku wake akaniambia mteja amekiuka masharti kwani amefanya sherehe na kupiga vigelegele, yani alikuwa anaumia sana na kujishika tumbo huku akisema wanamuumiza kwa kupiga vigelegele, nilikuwa naogopa sana. Mara akasema wanamuua kwa kukata keki, sikuelewa kabisa ila gafla niliona kimya na nilianza kupiga makelele ya kuomba msaada. Ila walipokuja kumuangalia waliona ameshakufa” Yule mwanamke akaangua tena kilio, basi Rose akawa anambembeleza huku akijlaumu moyoni kwani alijiona kuwa yeye ndio chanzo cha mambo yote hayo maana kama watoto wake wasingefanya ile sherehe basi yale yote yasingetokea. Ila hakusema hapo kuwa mteja mwenyewe mwenye majanga ndio yeye kwani aliogopa kusema na kuona kuwa atamuweka hasira huyu mama ukizingatia anaonekana alimuonya sana mume wake kuachana na kazi ya hatari kama yake. Rose alimfariji fariji pale mfiwa kisha akaaga na kuondoka na mwanae ila siku hiyo hata nguvu ya kusubiri pikipiki hawakuipata waliamua kutembea tu mpaka kwenye gari yao, na kwavile walikuwa na mawazo basi hata hawakuona kama ni mbali kutoka kule kwa mganga hadi walipoacha gari. Waliingia kwenye gari huku akili ya Rose ikiwa haifanyi kazi kabisa, “Lakini mama nilikwambia kuwa nina mashaka” “Mwanangu usiongee sana, hapa nimechanganyikiwa kabisa yani kabisa kabisa, unajua nimezini na marehemu!” “Kheeee umezini na marehemu?” “Tuache hizo habari, twende nyumbani tu. Nishachanyikiwa hapa” Rose alikuwa amechanganyikiwa kweli yani akili yake haikufanya kazi kabisa kwa muda huo, Ana alikuwa akimuhurumia tu mama ingawa alimuonya kabla ya yote. Rose alikuwa akiendesha gari kurudi nyumbani ila aligubikwa na mawazo mengi sana. Kwa upande wa Mishi, alishtuka akiwa nyumbani kwao wanampepea na aliposhtuka wote walimpa pole akauliza, “Nimefikaje hapa?” “Umeokotwa tu mwanangu na wasamalia wema ndio umeletwa muda sio mrefu, hivi ndio tulikuwa tunakupa huduma ya kwanza halafu tukuwaishe hospitali.” Mishi alijitahidi kuinuka na kumwambia mamake asiangaike na swala la hospitali, ingawa alikuwa na maumivu makali sana ila alijua ni maumivu ya kubakwa kwani tukio zima la usiku wake lilimjia kichwani mwake. Alijitahidi kwenda kuoga na kwenda kupumzika chumbani kwake ila mama yake alionekana kumuhurumia sana binti yake, ila Mishi alijiinamia tu chumbani kwake huku akikumbuka maneno ya Salome kuwa bora angekesha siku nzima pale akiomba msamaha kuliko kuondoka, “Kwani msichana anayechanganya wanaume nip eke yangu jamani! Kwanini kunipa laana ya hivi! Kwahiyo nimebakwa ndio furaha yao? Yani kama nimepata ukimwi nahakikisha nausambaza kwao, haiwezekani nikafanyiwa hivi. Kwanza Yule ni mtu wa aina gani wa kutoa laana kwangu? Ila dah nimekoma jana, sijui kama nitarudia. Najipa moyo tu” Aliwaza sana, hakutaka waende hospitali wala hakutaka kuwaeleza nyumbani kwao kilichompata, kwanza alishukuru Mungu kuzinduka kabla ya kupelekwa hospitali kwani kwa yeye ni aibu kubwa mno kusema kuwa alibakwa. Alitulia kidogo na kumuaga mama yake kuwa anaenda duka la madawa, “Kwanini usimuagize mtu mwanangu Mishi?” “Mama, mimi ni mzima, acha tu niende mwenyewe” Hakutaka kuagiza mtu kwani bado alihisi huenda mtu ambaye angemuagiza angejua tatizo lake, alifika duka la madawa na kununua dawa azitakazo ila wakati anarudi kwao, njiani akakutana na Salome na kumfanya ashtuke sana, “Mbona unashtuka hivyo Mishi? Umeona mzuka, mzimu au kitu gani?” “Aaaah hapana kitu” “Hukutegemea kuniona hapa eeeh!” Mishi alikuwa kimya tu kwani alianza kumuona Salome kama kidudu mtu kutokana na ile laana aliyompa jana yake, “Mishi, nimekuja kukupa ujumbe mmoja tu. Acha tabia yako hiyo, kama unahitaji mwanaume basi upate mwanaume akuoe na uwe mke wa mtu na utulie kwenye ndoa yako sio kutwa kucha kiguu na njia. Unawazibia wenzio liziki zao, wadada wenzio wapo wengi tu wakitaka wachumba halafu wewe bila aibu una miliki wote. Aibu umeipata kwa wachache tu wale, ila ukiendelea ipo siku nitakukutanisha na wanaume wote unaowachanganya, tulia upate mume” Mishi alimuangalia Salome kisha alijiuliza kimoyo moyo kuwa huyu binti mdogo hivi anajiamini nini mpaka kusema yale ila hakujua Salome anajiamini nini, hakumjibu kitu na kuanza kuondoka ila Salome akamwambia, “Ningekuwa ni wewe ningeuliza kuwa baada ya kubakwa kitanipata nini ili nikijua nianze kuchukua hatua ila kwavile wewe ni kiburi na mjuaji basi utakula jeuri yako” Salome akaondoka na kumfanya Mishi ajiulize sana, na moja kwa moja akahisi labda ni ukimwi. “Itabidi nikapime ukimwi, jamani katokea wapi binti Yule? Hata sijui kanijulia wapi” Mishi alirudi kwao ila akiwa na wazo la kwenda kupima ukimwi tu. Rose na mwanae Ana walifika nyumbani, kiukweli Rose alikuwa na mawazo sana. Walipoingia sebleni tu walimkuta Salome akiwa peke yake pale sebleni, na Walipoingia tu aliwapa pole ya msiba, Rose alimwangalia na kujiuliza kuwa amejuaje, ikabidi amuulize, "Pole ya msiba wa nani?" "Si wa mganga wako" "Halafu wewe Salome, nakuangalia tu muda mrefu. Siku zote nakuangalia tu, na utahama humu ndani mwangu" Kisha Rose akaondoka na Kwenda zake chumbani ila Salome alikuwa akicheka tu kiasi kwamba alimfanya Ana amuangalie kwa hasira sana, ila Salome alimuangalia pia Ana na kumwambia, "Na bado, mpaka mtaacha" Ana aliondoka na kuelekea chumbani kwake pia ila alijiuliza sana kuwa huyu Salome anajiamini kitu gani mpaka awe anacheka kwa dharau vile, kumbe mama yake nae alikuwa alijiuliza swala hilo hilo maana Ana aligundua baada ya kwenda kwa mama yake ili wakajadili vizuri na kumkuta mama yake akiongea, "Hivi huyu Salome anajiamini nini?" Ana aliingia na kumwambia mama yake kuwa hata yeye kitu hiko kinampa sana mawazo, na kumuuliza mama yake, "Tutamuweza kweli!" "Kwanini tusiweze wakati ni binadamu wa kawaida tu yule" "Kwahiyo tutafanyaje mama?" "itabidi tutumie nguvu, yani yule Salome tumtoe kwa nguvu maana bila hivyo atatushinda" "Sawa mama, ila je umeshajua kinachowamaliza waganga tunaowatafuta! Sio huyu huyu Salome kweli!" "Atatoa wapi nguvu za kufanya vitu vikubwa hivyo?" "Mama, hebu jaribu kufikiria kwanza. Unakumbuka jana asubuhi yule mganga alifika hapa kabla hujaenda kumfata halafu Salome akakuambia kuwa ni yeye ndio amemleta mganga yule, ukawa huru na kumuonyesha kila kitu, tumeenda kwake na kugundua alikufa juzi kwahiyo yule wa jana labda alikuwa mzimu au uliletewa marehemu bila kujijua" "Ana tafadhali mwanangu usiendelee kuongea, unanikumbusha machungu. Unajua yule mganga nimefanya nae vitu vingi sana, hadi nimeenda kumuonyesha ile nyumba yangu ya juu ambayo haikaliwi na mtu. Samahani kwa kukwambia haya mwanangu ila yule mganga nimezini nae" "Yani mama kwa swala hilo tambua kwamba umezini na marehemu, kuanzia leo hata sitaki tena mazoea na yule Salome, na amesema na bado mpaka tuache. Mama bado nina maswali mengi sana, Salome si mtu wa kawaida. Nitaendelea na dawa zangu mwenyewe nikishindwa basi ila kwa waganga wako siendi tena. Inaonyesha nao hawamuwezi" "Hutakiwi kukata tamaa mapema hivyo mwanangu, ngoja tutumie nguvu kwanza halafu kuna mganga wangu mwingine ndio kiboko kabisa" "Mama, siku ile yenyewe tulijaribu mikono ikaganda. Kwakweli sitaki tena" "Mwanangu naomba tujaribu mara ya mwisho tafadhali na sitokusumbua tena tikishindwa kwasasa" Rose alitumia muda wa ziada kumshawishi mwanae mpaka akakubali mipango ya mama yake. Wale mapacha pamoja na dada yao Sara hawakuwa na raha kabisa yani hata siku ile hawakutoka nyumbani kabisa, walikaa ndani tu kwahiyo hata muda ambao mama yao amerudi hawakumsikia sababu walikuwa na mawazo sana. Walikaa wote kwenye sebule ile nyingine huku wakijaribu kujadiliana. “Jamani mimi sijapendezewa kabisa na Yule Mishi kuondoka bila kumpiga kidogo” “Nyie ni wanaume ila wote mmemuogopa Salome alivyo mkingia kifua Yule Mishi, yani msichana simpendi Yule loh alifanya nione mapenzi machungu na nilie siku nzima ila ni Salome huyo huyo aliyenizuia kumpiga” “Ila hatuwezi jua jamani, labda tujipange namna ya kumshambulia Yule binti ila nitawaachia nyie, sina hamu nae mimi yani ananiambia kuna mahali anaenda kumbe analetwa kwetu kutambulishwa na ndugu yangu! Sina hamu nae Yule msichana kabisa” “Jamani nyie achene tu, nishapoteza hela zangu nyingi sana kwa Yule msichana na lazima nitamkomesha siwezi kukubali” Doto alionekana kuwa na hasira zaidi na Mishi sababu amejiona kama mjinga na alipata aibu jana ukizingatia ni yeye aliwaambia wenzie kuwa mchumba wake anakuja kumbe mchumba mwenyewe anajulikana na wote maana kashawaharibia mahusiano yao wote, Doto alikuwa na mpango kabambe kwa Mishi na hakutaka kushirikisha wenzie kwani hakutaka kuzuiwa kufanya anavyotaka yeye, kwahiyo walivyoongea ongea pale akawaaga wenzie kuwa anatoka kidogo nao hawakutaka kumuhoji zaidi. Doto aliondoka zake na safari yake ilikuwa ya kwenda kwakina Mishi, ambapo alifika na kuambiwa kuwa Mishi kalala ila aliomba kuongea nae, Mishi bila ya kujua kuwa ni nani alitoka ila alipomuona kuwa ni Doto akatamani kurudi ndani ila kwavile hakutaka kupata aibu pale kwao kuwa amegonganisha ndugu ikabidi atoke nae, aliposogea nae tu Doto hakuweza kuzungumza na Mishi kwanza kwani alijikuta akinyanyua mkono wake na kutaka kumzaba kofi ila cha kushangaza kabla ule mkono haujaangukia kwenye shavu la Mishi, Doto alijikuta yupo sebleni kwao halafu Salome akiwa mbele yake. Doto alishangaa sana, akajikuta akiuliza “Imekuwaje?” “Imekuwa hivyo hivyo ilivyokuwa, si nishawakataza kumpiga Mishi nyie! Kwanza na nyie mmeyataka wenyewe, wewe unakuwaje na mwanamke halafu pacha mwenzio humuonyeshi? Mnataka nini kama sio kutembeleana? NImesema Yule msichana asipigwe ila atapigwa na laana yangu, na nina maana kubwa sana kufanya hivi” Doto alimuangalia Salome kwa hasira sana kwani alionekana ni msichana mdogo ila aliyekuwa na amri zaidi, ila bado alikuwa hajielewi elewi hata alivyorudishwa nyumbani na kumuuliza swali Salome bado hakuelewa kabisa, akataka kutoka tena nje ila kabla hajatoka akamuona mama yake akiwa na Ana wakija kwa kasi sana na wameshika sufuria la maji ya moto na kummwagia Salome, ila muda huo huo alishangaa kuona kuwa yale maji kumbe alikuwa anamwagiwa yeye na sio Salome, alijikuta akipiga kelele za maumivu. Itaendelea kesho usiku…..!!!!! By, Atuganile Mwakalile.

at 4:47 PM

Bagikan ke

Lintaskan

0 comments:

Copyright © 2025 Braytonofficiallove
Designed by Siyamdezign | Edited By braytonofficiallove
braytonofficiallove | braytonofficiallove | braytonofficiallove
Powered By Blogger
Back to Top