KURUDI KWA MOZA: 32 Mlinzi alibeba kila kilicho chake kwani lengo lake lilikuwa ni kuondoka na kutokurudi tena kwenye nyumba hiyo, na kweli aliondoka eneo hilo na kwenda kupanda basi la kwenda kwao, ila alipofika tu stendi ya kwao na kushuka kwenye lile basi alijikuta yupo ndani kwenye nyumba ya Rose huku mizigo yake ikiwa pembeni. Alishangaa sana na kupatwa kama na sintofahamu maana ilikuwa ni kitu cha ajabu kwake ukizingatia alipanda gari la kwenda kwao na gafla anajikuta tena nyumbani kwa Rose, kwahiyo alikuwa akishangaa shangaa tu pale huku mizigo yake ikiwa pembeni. Salome alienda pale getini na kumshangaa pia halafu akamuuliza, “Vipi na mizigo?” “Yani sielewi, sielewi kabisa. Nilikuwa nishaondoka kwenye nyumba hii, nilishafika hadi stendi kwetu cha ajabu nimerudishwa tena hapa” “Nani kakurudisha sasa?” “Sijui ni nani, ila mimi mwenyewe nakumbuka kuwa mara ya mwisho nilikuwa stendi ya kwetu nashangaa nimerudi tena hapa. Kwanza saa hizi saa ngapi?” “Saa tisa, kwani vipi?” “Haya ni mambo ya ajabu sana, kutoka hapa hadi kufika kwetu ni masaa saba, ni kweli hapa nimetoka saa mbili asubuhi ila nimerudishwa kwa sekunde jamani, hii si haki yani hata kijijini kwetu sikufika, nilifika tu mkoani. Hili swala sio haki kabisa” “Sasa nani kakufanyia hivyo?” “Sijui ila natamani nifike kwetu jamani, nimechoka mimi na maajabu ya nyumba hii” “Unatakiwa tu uwe mvumilivu, utapoteza nauli bure tu. Wewe tulia na usifikirie kila anayerudishwa hapa ni mchawi, je wewe ni mchawi?” Akakumbuka jana yake aliwaambia watu wa humo ndani wote wachawi kwasababu alikuwa anawaona kutoka halafu hawaoni kuingia ila leo jambo hilo lilikuwa limempata yeye, akaona kwa staili ile ni ngumu kwake kuondoka ila hapo hapo alipata wazo la kuwasiliana na kwao ili awaeleze kuhusu tatizo hilo maana limekuwa kubwa sana kwa upande wake. Rose baada ya mlinzi wake kuondoka asubuhi ya siku hiyo, na yeye alifanya safari ya kumtafuta mganga wake aliyemfikiria kichwani, alimtafuta sana bila ya mafanikio ila njiani akakutana na rafiki yake wa muda mrefu sana ambaye aliwahi kumshauri kuhusu swala la waganga kwahiyo alivyokutana nae alifurahia sana, na kuanza kumshirikisha kuhusu swala lake linalomsumbua kichwa. “Basi mwezi uliopita mwenzio nilipatwa majanga hayo balaa, yani kuna mavitu yalichanganya kichwa change kama nini ila kuna kijana huyo ni matata, kwanza kijana haogopi kitu yani hakuna takataka yoyote inayomshinda. Huyo kijana ni kimbilio la watu wengi sana, wanaotafuta watoto, wanaotafuta mali yani kila kitu. Nina uhakika huyo kijana hawezi kushindwa, hao waganga wako wamechoka halafu waoga” “Huyo atakuwa mzuri kweli, nilijaribu kumtafuta hata Yule wa mwanzo aliyewahi kunipa dawa ya kufukia ndani kwangu ila sijampata” “Unadhani Yule unampata kirahisi hivyo? Yule hakuwa mganga ni jinni lile, na anapatikana kwa waganga wanaojiweza tu, Yule mganga tuliyeenda kipindi kile alikuwa anajiweza ndiomana ikawa rahisi kukutana na Yule wa dawa. Ingawa masharti mengi umeyavuruga ila kwa Yule ndio kiboko” “Naomba nipeleke ndugu yangu, nipo tayari kutoa kitu chochote kile ila niepukane na aibu hii maana kwangu ni aibu na fedheha” Basi huyu rafiki wa Rose akajitolea kumpeleka Rose, na kwavile alimuomba ampeleke siku hiyo hiyo akajitolea kufanya hivyo ingawa ni mbali sana hiyo sehemu. Patrick hakujisikia kuondoka kabisa nyumbani kwa Neema, na alichofanya Salome ni kwenda kumchukulia Patrick nguo zake zote na kumfanya afurahi zaidi kurudi kwa Neema, alimuomba Neema asimfukuze eneo hilo kwani alizidi kufunguka mawazo ya kuhusu mali zake na nyumba zake ambazo zingine alikuwa hata haendi kuzitembelea kwavile alishazisahau ila Neema akawa kama amemkumbusha kwahiyo alifurahi sana kumalizia muda wake kwa Neema, na pia watoto wale mapacha wa Neema aliwaona ila aliogopa kuuliza kuwa wale watoto ni wa nani, ila alijikaza na kuuliza, “Samahani Neema, na hawa watoto wako wengine baba yao yuko wapi?” Neema akacheka kisha akamwambia, “Baba yao ni wewe” “Ni mimi? Kivipi?” “Najua huwezi kukumbuka au kujua, hii kitu niliiweka siri siku zote za maisha yangu” “Niambie kivipi?” Basi Neema ilibidi amueleze Patrick ilivyokuwa, “Kuna kipindi nilikuwa nauza baa, na ulikuja kunywa sijui ulikuwa na mawazo gani ila ulikunywa sana hadi ulilewa. Ikawa kila mwanamke anayepita mbele yako unamshika, ilibidi nidanganye kuwa umenihitaji mimi na kwenda na wewe chumbani, ila kwa nguvu ya pombe uling’ang’aniza kulala na mimi, kwavile nilikuwa bado nakupenda sikuweza kukataa, nililala na wewe ila usiku wake niliondoka na kukuacha umelala fofofo. Kulipokucha uliondoka halafu na mimi niliacha kazi pale kwenye ile baa, sikuwahi kumwambia mtu yeyote kilichotokea baina yangu na yako, na baada ya mwezi nilijigundua kuwa nina ujauzito hapo ndipo nilipoamua kufanya siri hadi nimejifungua. Ilikuwa ni siri yangu hata ndugu yangu Yule Ashura sikuwahi kumwambia chochote, ingawa sasa nimegundua hakuwa ndugu yangu, yani kama hakuwa ndugu yangu alikuwa na mipango gani kwangu? Ni siri yake kwakweli, ila hakuwahi kujua kuwa watoto wangu ni wa nani sababu mar azote alizoniuliza nilimwambia kuwa nilibakwa” Patrick alishangaa sana hii habari, na kujaribu kuvuta kumbukumbu ya siku aliyolewa sana, alikumbuka tu kuna siku alilewa sana ila hakukumbuka ni kitu gani alikifanya, “Na hiyo siku niliyolewa sana ndio siku iliyobadilisha maisha yangu kabisa, maana tangu siku hiyo niliporudi nyumbani ndio nikafanywa kama ndondocha yani sikuwa na uwezo wa kwenda sehemu yoyote ile bila ruhusa ya Rose, yani kipindi hiko ndio mateso yalizidi kwangu maradufu” “Pole sana, basi hivyo ndivyo ilivyokuwa kuhusu hawa watoto. Yani ni wanao kabisa” “Kwakweli nimeteseka sana mimi, siku ile ilipelekea kunywa sana pombe baada ya kumuona mke wangu akiniwekea dawa kwa macho yangu, mimi sio mlevi kiasi kile ila siku ile nililewa sababu ya mawazo. Ila kitendo cha kurudi nyumbani ndio nikawa ndondocha kabisa, yani hakuna kitu nilichokuwa nafanya kwa akili yangu.” Patrick aliomba aitiwe watoto wale ili awaangalie kwa karibu maana hakuamini amini kuwa alikuwa na watoto, maana alijua kuhusu Salome ila hakujua kama ana watoto wengine. Neema aliwaita watoto wake, nae Patrick aliwakumbatia kwa furaha hata wale watoto walibaki kushangaa tu kwani hawakutegemea huyo mtu kuwafurahia kiasi kile tena huku akiwaita wanangu, walikuwa wakishangaa shangaa tu ikabidi Neema awaambie, “Baba yenu huyo” Na wao wakashangaa na kufurahi maana hawakufikiria kutambulishwa baba, kwani siku zote walipokuwa wakiulizia kuhusu baba yao Neema alikuwa akiwafokea sana. Patrick akazidi kupata uchungu dhidi ya Rose na mali zake, ilimuuma sana na kumfanya sasa awaze namna ya kurudisha mali zake kwenye mikono yake ili watoto wake wafaidi. Ana alishaamua kujitoa kabisa kwenye maswala ya waganga na kumkataza mama yake kwa kadri awezavyo lakini mama yake alikuwa mbishi sana, yeye Ana alikuwa na uwezo wa kupata hisia za mama yake alipoenda kwahiyo siku hiyo akapata hisia kuwa mama yake kaenda tena kwa mganga ila inaonyesha wazi alishindwa kumuaga sababu alijua angemzuia. Ana alikuwa chumbani kwake, alifunua godoro lake na kutoa dawa yake, kwa mara ya kwanza aliamua kutumia dawa yake ili avuruge akili ya mama yake na kumfanya arudi nyumbani na ili aweze kubaini ni nani anaewaumiza kwenye nyumba yao. Aliamua kwanza abaini ane waumiza katika nyumba yao, “Jitokeze nikuone wewe unayetusumbua humu ndani” Alisema maneno hayo kama mara tatu na gafla alihisi kuna mtu kasimama mbele yake, aliinua kichwa chake huku amejawa hofu ila alijitia ujasiri na kumtazama mtu huyo, alikuwa ni Moza kwakweli Ana alishtuka sana na kumfanya ashindwe hata kumuuliza chochote zaidi ya kutetemeka tu. Moza alimuangalia Ana na kucheka ila Ana hakuweza kumtazama zaidi Moza, na badala yake alijikuta akizimia tu pale ndani kwake. Muda huu Sara alikuwa nje ya chumba cha Ana akigonga na aligonga kwa muda mrefu sana bila ya kufunguliwa hadi ikabidi afungue mwenyewe, alishtuka sana alipoingia ndani kwani alimuona Ana akiwa kajifunika makhanga halafu kuna kitu pembeni yake ambacho alikishangaa sana Sara kwani hajawahi kuona kitu cha namna ile tangia azaliwe, alipiga kelele na kumfanya kaka yao Kulwa aje ndani pia ila alishangaa alichokiona pembezoni mwa Ana muda huo Ana akiwa kazimia, alimshika mkono Sara na kumtoa nje haraka haraka kisha kumwambia, “Yule mdogo wetu ni mchawi, yani bila ubishi Yule ni mchawi, sasa ndugu yangu maswala ya kumfatilia mchawi ni maswala mazito sana. Pale tunamuona kama kaanguka ila huwezi jua labda ameenda kwenye uchawi wake utashtukia anashtuka na kuanza na wewe, tukae mbali dada yangu tunaishi na nyoka humu ndani” Sara hakuweza hata kuchangia hoja kwani kiukweli mambo ya nyumbani kwao yalimchosha tena sana tu ila hakuwa na jinsi na hakuwa na pakukimbilia, muda kidogo Salome nae alitokea nje na kuwafata sebleni Sara na kaka yake kisha kuwauliza kuwa kuna nini, ila Sara nae alimuuliza, “Hili hujalijua au?” “Ningelijua ningeuliza?” “Na sisi hatujui kuna nini” Salome alicheka kisha akaelekea njia ya vyumbani, ila Sara alimuangalia sana Salome kwani siku hizi alianza kuwa na mashaka nae pia. Rose kule alipopelekwa kwa mganga walifika jioni kabisa karibia na usiku hata hivyo mganga mwenyewe hawakumkuta, ni baadae ambapo giza lilikuwa limeingia kabisa ndio alirudi na kukuta kuwa anangojwa kwa hamu zote. Rose alitaka kuhudumiwa usiku huo huo ingawa Yule mganga pia alikataa kumuhudumia kwa usiku huo kutokana na mlolongo wa matatizo yake. “Labda tuanze tiba saa nane usiku” “Nipo tayari hata saa ngapi ila hili jambo liishe, nateseka sana” “Litaisha tu, hapa ndio mwisho wa matatizo yote” Rose alisubiri kwa hamu zote hata kulala kidogo hakutaka, rafiki yake aliyempeleka aliamua kuondoka na kumuacha Rose muda uleule, kwahiyo Rose alibaki peke yake kwa Yule mganga huku akisubiri tiba, hakujali kukoje kukoje kule ila alichojali yeye ni kupata tiba tu. Rafiki wa Rose alijulikana kwa jina la mama Jack, muda aliokuwa anarudi kwake ni usiku tayari ulishaingia kutokana na kwake kuwa mbali kidogo na kwa mganga huyo, ingawa alitumia usafiri wa kukodi ila alichelewa sana kufika nyumbani kwake. Alipofika tu alimuona mtu yupo pembezoni mwa nyumba yake akilia kanakwamba ni mtu aliyekuwa na shida, alipomuangalia alimuona ni binti mdogo tu, alimfata na kumuuliza tatizo, “Vipi binti?” “Nimefukuzwa na mama wa kambo” Huku Yule binti akiendelea kulia, mpaka mama Jack alimuonea huruma kwani alijua wazi kuwa ikiwa atamuacha hapo nje binti huyo anaweza kubakwa na vijana wasio na huruma kwahiyo alimwambia aingie nae ndani kisha kuzungumza nae na kumuahidi kuwa kesho atamsaidia afike kwa mama yake. Yule binti alikubali na kumshukuru sana huyu mama, kisha Yule mama akamuandalia sehemu ya kulala binti Yule. Hakuwahi kumuona, hakuwahi kumfahamu ila ni huruma tu ndio iliyomfanya amsaidie. Yule binti alionyesha kumshukuru sana Yule mama kiasi cha kumfanya Yule mama ajisikie vizuri na ajione kuwa katenda jambo jema sana kumsaidia Yule binti. Ilipofika saa nane usiku Yule mganga alianza kufanya dawa zake, Rose alikuwa macho kabisa kwani alitaka kwanza kushuhudia anavyofanyiwa dawa. Yule mganga alijifungia kwa mud, kisha akatoka na kumwambia Rose, “Unahisi ni nani anayekufanyia mambo ya ajabu?” “Ni Yule binti Salome, sijui kapata wapi uchawi” “Hapana, anayekuchezea wewe ni Moza” Rose alishtuka na kumuuliza mganga kwa mshangao, “Moza” “Ndio Moza, amerudi kwa lengo moja tu la kukutesa wewe” “Kwahiyo Moza alikufa na kurudi?” “Hapana, Moza hakufa kama unavyofikiria ila Yule unayemsema Salome si Salome ni Moza Yule. Nimekwambia amerudi kwa kasi ya ajabu” “Kheee, kwahiyo Salome yuko wapi?” “Salome yupo mahali na amelala usingizi mzito sana, si mimi wala si wewe tunaoweza kumuamsha labda Moza mwenyewe apende kumuamsha na atamuamsha endapo azma yake ikikamilika” “Mmmh ana azma gani kwangu?” “Anataka uwaachie wale watu uliowafungia kwenye kichumba” “Mmmh siwezi mganga, itanigharimu maisha yangu yote, siwezi” “Anatambua hilo kuwa itakugharimu maisha yako yote ndiomana anataka wewe mwenyewe uwatoe, huyu Moza ni amejipanga yani amejipanga haswaaaa” “Sasa nitafanyaje?” “Inahitajika kafara” “Nipo tayari kuwatoa kafara wale niliowafuga” “Hapana hawatakiwi hao, kafara inayohitajika ni kafara ya mtoto wako” Rose alipata hofu kusikia habari ya kutoa mtoto wake kafara tena, uoga ulimshika kwani hakutaka kuona mtoto wake yeyote anakufa kwaajili yake. “Hakuna njia nyingine?” “Hakuna, zaidi ya kutoa kafara. Ikiwa unahitaji kuendelea kubaki kwenye nafasi yako, toa mtoto wako kafara” “Mmmh sasa nitamtoa mtoto wangu gani?” “Mtoe mwanao wa hospitali, kwani itakuwa rahisi sana kusema kuwa kafia hospitali sababu ya kuungua maji moto” Kidogo maneno ya huyu mganga yalikuwa yakimuingia vilivyo Rose na kuanza kuhisi kuwa huyu mganga ni mkweli, akafikiria kuhusu mwanae Doto ila badae akaona ni vyema kumtoa kafara mwanae Yule mmoja na kuokoa maisha yake na maisha ya watoto wake wengine, akamkubalia mganga na kusubiria maelekezo atakayompa. Ila mganga alikubaliana nae kumpa masharti asubuhi ya siku inayofuata. Asubuhi yake, mganga alimtaka Rose kwenda mtoni na kumwambia kuwa huko ndiko ambako ataenda kutoa kafara, kuna dawa alimpa na kumwambia kuwa ataenda kuinyunyiza mtoni halafu kingetokea kitanda cha hospitali ambacho kalazwa Doto kisha kitanda hicho akisukumie mtoni hapo atakuwa amefanikiwa na kumtoa kafara mtoto wake, Rose aliona hilo swala ni jepesi kwake kwani halikuwa sharti gumu kumfanya shindwe kulitekeleza, kwahiyo alichukua hiyo dawa na kuanza safari ya kwenda mtoni. Alivyofika mtoni alimwaga dawa ile kwenye mto, ni kweli kikatokea kitanda pembeni na alipoangalia aliyelala kwenye kitanda hicho hakuwa Doto bali alikuwa ni Moza. Itaendelea Jumatatu usiku…..!!! By, Atuganile Mwakalile.

at 4:49 PM

Bagikan ke

Lintaskan

0 comments:

Copyright © 2025 Braytonofficiallove
Designed by Siyamdezign | Edited By braytonofficiallove
braytonofficiallove | braytonofficiallove | braytonofficiallove
Powered By Blogger
Back to Top