MAPENZI YA FACEBOOK-11 Sikutaka kukurupuka katika kufanya maamuzi, niliamua kutumia akili katika suala hilo. Niliamini facebook matapeli walikuwa ni wengi sana hivyo sikutakiwa kumuamini Juliet kupitiliza. Kitu nilichoamua kukifanya ni kumpigia simu na kutaka kuisikia sauti yake, nilitamani sana kumsikia alifananaje sauti. Nilipiga simu yake lakini ajabu haikuwa ikipokelewa kabisa jambo lililonishangaza sana. “Itawezekanaje?” nilijiuliza mara baada ya kupiga simu zaidi ya mara tatu bila kupokelewa. Niliamua kumtumia ujumbe mfupi lakini alionekana kuwa kimya. “Mbona hupokei simu?” (Kimya!) “Juliet!” (Kimya!) Nilizidi kuwa katika wasiwasi mkubwa sana, sikujua ni nini kilichokuwa kimetokea mpaka Juliet akashindwa kuipokea simu yangu. Ama kweli jambo usilolijua ni sawa sawa na usiku wa kiza kinene, nilikuwa katika kiza ambacho sikuwa nikifahamu ukweli wa kile kilichokuwa kinaendelea katika maisha yangu. Mbali na kumfahamu Juliet facebook na kuweza kupata namba zake lakini kiukweli hakukuwahi kutokea siku nikaweza kuzungumza naye kwenye simu, kila nilipokuwa nikimpigia simu alikuwa akiikata na kudai kuwa ilikuwa mbovu hivyo alinitaka tuchat jambo ambalo kiukweli lilikuwa likiniweka katika wakati mgumu sana. “Kwanini hutaki kupokea simu yangu?” “Simu yangu mbovu tuchat tu!” “Kwahiyo hatuwezi kuongea?” “Ndiyo mpenzi,” alinijibu jibu ambalo kiukweli lilinifanya nishangae kwa kiasi fulani, yani sikuwa nimemtongoza wala kumtamkia neno lolote la kimapenzi sasa ilikuwaje nikawa mpenzi wake. Hilo lilizidi kunishangaza sana. Nikayakumbuka maneno ya Juma kuwa facebook hakukuwa na mapenzi ya kweli zaidi ya uwongo mwisho wa siku kuumiza. Sikutaka kukubaliana naye kabisa yani kwa jinsi Juliet alivyokuwa akionekana kuwa msichana mrembo sikutaka kukubaliana na maneno yake kabisa, nilihisi alikuwa akiniongopea. Niliamua kumuambia ukweli wa hisia zangu Juliet, sikutaka kumficha chochote kile nilichokuwa nikikihisi. Nilidhamiria kuwa naye katika maisha yangu. “Nakupenda Juliet.” “Unanipenda?” “Ndiyo.” “Unanipendea nini?” “Nakosa jibu la kukujibu ila nimetokea kukupenda tu!” “Siunajua mimi ni mwanamke ambaye ninahitaji matunzo.” “Ndiyo nafahamu.” “Utaweza kunihudumia, kunisomesha pamoja na kunilipia pango la chumba?” “Ndiyo nitaweza ondoa shaka mrembo.” “Sawa nimekukubalia ombi lako.” “Nimefurahi sana kwa kunikubalia ombi langu, nakupenda sana.” “Nakupenda pia Phidelis wangu.” Kwa kipindi chote hicho sikuwahi kuongea na Juliet na mara zote nilipokuwa nikitaka kuzumgumza naye alikuwa akiweka vipingamizi vingi, sikujua ni kwanini alikuwa akiweka vipingamizi hivyo hata pale nilipotaka kukutana naye aliweza kunikatalia na kuniambia kuwa nipange siku maamulu ambayo nitaweza kwenda kuonana naye. Urafiki wetu ulianzia facebook, urafiki ambao ulikuja kuzaa mapenzi ambayo kiukweli nilijikuta nikiwa katika mahusiano ilihali sikuwahi kuonana naye kabisa, yalikuwa ni mapenzi ya facebook tu! kutumiana picha pamoja na kusifiana. Hata pale lilipokuja suala la kumtumia pesa, nilimtumia bila kusita, niliamini alikuwa ni mwanamke ambaye alikuwa akinipenda sana kuliko kitu chochote kile. Niliamua kumtumia pesa ya pango ya chumba aliyokuwa akidaiwa pamoja na ada ya chuo. Mapenzi yetu yalibakia kuwa ya facebook tu! mpaka pale siku moja nilipokuja kupata habari iliyokuwa ikitangazwa na kuchapishwa katika magazeti mbalimbali kuhusiana na taarifa za shoga ambaye alikuwa akitumia jina la Juliet mitandaoni kutapeli wanaume. Kwa kweli sikutaka kuamini kile nilichokuwa nikikiona katika magazeti ya siku hiyo. **** “SHOGA ANAYETUMIA JINA LA JULIET AZIDI KULIZA WENGI FACEBOOK!” Kilikuwa ni kichwa cha habari cha gazeti moja ambalo nilikuwa nikilisoma. Katika gazeti hilo ilikuwepo picha ya mwanaume mmoja mwenye asili ya shombeshombe pamoja na picha ya mwanamke. Niliitazama kwa umakini wa hali ya juu ile picha ya yule mwanamke. Naam! Hakuwa mgeni machoni mwangu. Alikuwa ni Juliet mwanamke aliyetokea kunichanganya katika mapenzi kiasi kwamba nikawa sioni wala sisikii lolote juu yake. “Juliet!” nilijikuta nikiita kwa kushtuka. Sikutaka kuamini kile nilichokuwa nikikisoma katika gazeti, Juliet hakuwa ni mwanamke kama nilivyokuwa nikidhani. Alikuwa ni yule shoga ambaye alikuwa akitumia picha ya mwanamke Facebook ili aweze kuwatapeli wanaume. Naam! Ni kweli alifanikiwa katika mpango huo, aliweza kuwaliza wanaume wengi sana kutokana na uzuri aliyokuwa nao mwanamke yule. Miongoni mwa wanaume waliyolizwa siwezi kupinga nilikuwa ni miongoni mwao. “Siamini kwa kweli kumbe Juliet si mwanamke ni shoga?”nilijiuliza swali lililonifanya nisiamini kabisa habari ile niliyokuwa nikiisoma katika gazeti. Nilichoamua kukifanya ni kuichukua simu yangu kisha nikaingia Facebook ili niweze kukiaminisha kile nilichokuwa nikikisoma. Nilipoingia kitu cha kwanza niliingia upande wa kutafuta majina. Nililiandiika jina la Juliet kisha nikaanza kutazama picha ya yule mwanamke ambayo ilikuwa imewekwa katika akaunti hiyo. Kitu kilichonishangaza hakukuwa na picha katika akaunti ya Juliet, ilikuwa imetolewa. Sikutaka kuamini nikaamua kumtumia ujumbe mfupi lakini nilipotaka kufanya hivyo nilishindwa, alikuwa ameniblock. Kwa kweli nilihisi kuchanganyikiwa ndugu yangu, kuna kipindi nilihisi nilikuwa nikiyaona mapichapicha tu, sikutaka kuamini kabisa kama nilikuwa nimetapeliwa tena na shoga wa Facebook. Niliyakumbuka maneno ya rafiki yangu Juma aliyowahi kuniambia kuhusu Facebook, hakika yalionekana kuniingia vyema. Nilitamani kuzirudisha siku nyuma ili niweze kujitoa katika penzi la na Juliet lakini lilikuwa ni jambo gumu kutokea. Majuto yalikuwa kwangu, nilizidi kujiona mjinga sana hasa baada ya kusalitiwa na mke wangu kisha na mimi kuamua kulipiza kisasi katika mtandao huu ambapo nilijikuta nikiangukia kwa shoga ambaye nilikuwa nikimuhudumia kama mke wangu wa ndoa. Tukio hilo lilizidi kuniumiza sana, kumbukumbu hiyo ilinitesa sana katika maisha yangu. Niliamua kumuambia Juma ukweli wa kile kilichokuwa kimetokea. “Umeona umeona?” aliniambia baada ya kumuelezea ukweli wa kile kilichokuwa kimetokea. “Yani ndugu yangu we acha tu!” “Lakini nilikuambia mimi.” “Juma yani siamini.” “Huamini nini sasa, we endelea kuhudumia,” aliniambia huku akinicheka, kicheko ambacho kilinifanya nijisikie vibaya. “Sasa unanicheka.” “Tatizo lako wewe husikii.” “Nimekoma.” “Sasa ndiyo ujifunze,” aliniambia huku akionekana kufurahishwa na tukio lile. Facebook ilinipa funzo katika maisha yangu, sikutakiwa kumuamini mtu bila sababu za msingi katika mtandao huu, ni hapa ambapo niliamini kuwa kuna baadhi ya watumiaji wa facebook walikuwa wakipenda kutumia picha ambazo zilikuwa si zao. Unakuta mtu anaitwa Revocatius Kisoka lakini facebook kaweka picha ya Chris Brown au msichana unakuta kaweka picha ambayo si yake halisi. Hili ndilo lililowahi kunitokea, mapenzi ya facebook yalinipa funzo kubwa mno. Kuna kipindi nilimuona msichana mwingine facebook, huyu alikuwa akiitwa Cleopatra Mushi lakini kwa facebook alikuwa akitumia jina la Precious Girl, kwa kweli alinivutia sana lakini kila nilipokuwa nikiyakumbuka yale yaliyowahi kunitokea katika maisha yangu ya facebook, niliogopa kumtongoza japo tulikwishaanza kuchat lakini niliamua kumpotezea. Nimeamua kuishi maisha yangu mpaka pale siku nitakapopata mwanamke ambaye atakuja kunipenda kwa dhati. Aweze kuliziba pengo aliloliacha mke wangu.” Alimaliza kusimulia Phidelis. MWISHO. Huu ndiyo mwisho wa simulizi yetu ya Mapenzi ya Facebook. Je, ni nini kilichokuvutia, una lipi la kunishauri katika simulizi hii na ni kipi ulichojifunza? Aidha nipende kuwashukuru marafiki zangu Phidelis na Revocatius kwa kuniruhusu kuyatumia majina yao katika simulizi hii. Pia nipende kuwashukuru nyote mliyokuwa nami kuanzia mwanzo mpaka mwisho wa simulizi hii . 🙏🏻🙏🏻🙏🏻🙏🏻🙏🏻🙏🏻🙏🏻🙏🏻 #Kumbuka kushare page hii kwa marafiki ili na wao waweze kuilike pae hii. Ahsanteni.

at 12:46 PM

Bagikan ke

Lintaskan

0 comments:

Copyright © 2025 Braytonofficiallove
Designed by Siyamdezign | Edited By braytonofficiallove
braytonofficiallove | braytonofficiallove | braytonofficiallove
Powered By Blogger
Back to Top