MAPENZI YA FACEBOOK-10 Moyo wangu ulikuwa na kisasi kikubwa sana. Tukio la kushuhudia ndoa ya Ester hakika liliniumiza sana. Nilijitahidi kuvumilia maumivu niliyokuwa nikiyapata lakini nilishindwa kabisa. Picha zake na mume wake alizokuwa akizipost zilizosindikizwa na maneno yaliyokuwa yakinilenga kwa asilimia mia moja, zilizidi kuniumiza sana moyoni mwangu, nilihisi maumivu yasiyomithilika. “Ina maana alikuwa hanipendi, sasa kama alikuwa hanipendi si angesema ili nisifunge ndoa naye?” nilijiuliza swali lililokosa jibu kabisa. Nilizidi kuwa katika wakati mgumu sana katika maisha yangu. Maisha yangu yalibadilika kwa kiasi kikubwa sana, nilikuwa ni mtu wa kuwaza kila wakati, kula, kunywa, kuvaa hata wakati mwingine kulala kwangu ilikuwa ni tabu, sikuwa mtu wa kwenda tena katika mihangaiko yangu, niliishi kwa kuteseka sana. Kuna kipindi nilitamani kumuomba msamaha Ester na kumuambia kuwa kile kilichokuwa kimetokea kati yetu niliamua kusamehe hivyo tulitakiwa kuishi kama zamani. Hilo lilikuwa jambo gumu sana kulifanya, niliamini sikutakiwa kulifanya hata kidogo. Niliamua kuingia facebook na kuanza kumtafuta msichana ambaye niliamini ningeweza kumuoa kabisa ikiwa ni katika harakati za kutaka kulipiza kisasi, niliamini kwa kufanya hivyo nilikuwa naenda kuuridhisha moyo wangu, moyo ambao ulisalitiwa, uliumizwa na Ester mwanamke ambaye alinidhihaki katika ulimwengu wa mapenzi. Nilipoingia katika akaunti yangu ya facebook kazi yangu kubwa ilikuwa ni kuongeza idadi ya marafiki, nilikuwa nikiongeza marafiki huku wengi wao wakiwa ni wasichana. Niliwaomba urafiki wasichana wengine ambao kiukweli nilikuwa siwafahamu kabisa. Msichana wa kwanza kabisa kunikubalia ombi langu la urafiki alijulikana kwa jina la Juliet Dickson, alionekana kuwa msichana mrembo sana, macho yake ya kurembua, sura ya kitoto iliyosindikizwa na umbo lake matata lilizidi kumfanya aonekane kuwa msichana mrembo sana, alikuwa akivutia kutazama. Niliingia katika akaunti yake na kuanza kupekuwa baadhi ya picha mbalimbali alizowahi kuzipost. Kwa kweli alinivutia sana na hii ndiyo sababu iliyonifanya nikaamua kumuomba urafiki kitendo ambacho hakikuchukua muda akaweza kunikubalia ombi langu. Nilipomuangalia, alionekana kuwa online kwa wakati huo. Sikutaka kupoteza muda kabisa nikaamua kumtumia ujumbe mfupi. “Asante kwa kunikubalia ombi langu.” “Usijali karibu.” “Asante mrembo?” “Sawa.” “Vipi lakini?” “Safi tu!” “We ni mrembo sana, unavutia kwa kweli.” “Asante kaka yangu.” “Maisha yanasemaje?” “Yako poa?” “Uko pande zipi?” “Dar.” “Dar kubwa lakini.” “Nipo Sinza.” “Sinza ipi?” “Sinza makaburini.” “Nashukuru kufahamu.” “Usijali na wewe?” “Mimi niko temeke tandika.” “Ooh! Sawa,” alijibu Juliet na huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa urafiki wetu. Juliet alitokea kuuteka moyo wangu, nilijikuta nikianza kumpenda kwa mara ya kwanza baada ya kuziona picha zake. Sikutaka kuamini licha ya uzuri aliyokuwa nao eti! alikuwa ameolewa, nilijiaminisha kuwa alikuwa bado hajaolewa na hivyo ni mimi pekee ambaye nilitakiwa kumuoa. “Lazima nimkamate Juliet,” nilijisemea huku nikizitazama picha zake, alikuwa akivutia sana. Nilichokuwa nakiamini ni mapenzi ya kweli niliyokuwa nikiyatafuta facebook, niliamini kwa muonekano wangu nisingeweza kukosa mwanamke ambaye angeweza kunipenda na kuiziba nafasi aliyoiacha mke wangu. Niliamini katika mapenzi ya kweli ambayo ningeweza kuyapata ila naweza kusema ilikuwa tofauti na kile nilichokuwa nakitegemea. Ama kwa hakika mapenzi ya facebook yameniacha na funzo kubwa katika maisha yangu. **** Facebook! Facebook! Kama sio facebook leo nisingeamua kukusimulia simulizi hii ambayo itakwenda kukuacha na funzo kubwa katika maisha yako. Nilipoanza urafiki na Juliet, hakuonekana kabisa kujali urafiki huo japo mara kwa mara nilikuwa nikilike pamoja na kukomenti picha zake. Niliutumia muda wangu mwingi sana katika kuchat na Juliet huku nikiamini mwisho wa siku nitafanikiwa kuwa naye kimapenzi. “Umependeza sana.” “Asante phidelis.” “Za masiku?” “Nzuri tu.” “Hivi ulisema unaishi wapi vile?” niliuliza swali la kinafki huku nikiwa nafahamu vizuri.” “Jomoni ndiyo umesahau mara hii?” “Ndiyo sababu nikakuuliza.” “Sinza makaburini.” “Unafanya kazi gani?” “Mbona mapema hivyo jamani.” “Kwani kuna ubaya wa mimi kufahamu?” “Hapana hakuna ubaya.” “Basi niambie.” “Mimi mwanafunzi.” “Mwanafunzi wa shule ya msingi, sekondari au?” “Nipo chuo.” “Chuo gani?” “UDSM.” “Vizuri sana hivi unasomea nini?” “Kaka naona maswali yamekuwa mengi kama polisi kwaheri,” alinijibu Juliet na huo ndiyo ulikuwa mwisho wa kujibu jumbe zangu. Nilijisikia vibaya sana hasa baada ya Juliet kunijibu hivyo , sikutaka kuishia hapo niliamua kumtumia ujumbe mfupi lakini hakuweza kunijibu chochote, alionekana kuwa online kwa wakati huo lakini ni kama vile alikuwa hajali jumbe zangu nilizokuwa namtumia. “Juliet mbona kimya sasa.” (Kimya!) “Juliet!” (Kimya!) “Mrembo?” (Kimya!) Nilizidi kutuma ujumbe lakini hakuna jibu lolote nililoweza kuambulia. Hakuna siku niliyoweza kujisikia vibaya kama siku hiyo. Nilikuwa nikimpenda sana Juliet japo sikuwahi kukutana naye lakini alionekana kunivutia sana katika maisha yangu. Nilitamani nipate muda wa kuweza kuongea naye ili niweze kumwambia dhamira yangu kwake lakini nilishindwa. Nilizidi kumsumbua kila siku lakini ni kama vile nilikuwa nikitwanga maji kwenye kinu, hakuna chochote nilichoweza kuambulia zaidi ya ukimya ambayo ulitawala. Niliichukua moja ya picha ya Juliet na kuisave wallpaper katika simu yangu. Alionekana kuvutia sana. Kila nilipokuwa nikimtazama moyo wangu ulihisi kufarijika sana. **** Niliamua kumueleza kila kitu rafiki yangu Juma kuhusu Juliet na kwa jinsi nilivyokuwa nikimpenda kutoka moyoni mwangu, nakumbuka jibu kubwa alilonijibu ni kuwa facebook hakuna mapenzi ya kweli. Hilo sikutaka kukubaliana naye kabisa. “Rafiki yangu facebook hakuna mapenzi,” aliniambia Juma, wakati alikuwa nyumbani kwangu Tandika Azimio majira ya saa kumi jioni. “Lakini anaonekana kuwa mrembo sana.” “Kuwa mrembo sio tatizo Phidelis halafu mbona wanawake wako wengi tu kwanini unang’ang’ania huko facebook.” “Juma wewe unaongea tu hivi kwanza umemuona huyo Juliet mwenyewe?” nilimuuliza. “Yuko wapi?” aliniuliza huku akionekana kuwa na hamu ya kutaka kumuona, niliamua kumuonyesha picha yake. “Mtoto huyo hapo,” nilimuambia huku nikimuonyesha. “Hahaha! Kwahiyo ndiyo umeamua mpaka kumsave kwenye simu yako?” “Nampenda.” “Anajua?” aliniuliza swali lililoniweka katika wakati mgumu wa majibu, ni ukweli usopingika kuwa mpaka kufikia wakati ule sikuwa nimeweza kuzungumza na Juliet habari zozote kuhusu mapenzi, nilijivika vazi la mapenzi ili hali muhusika hata hakuwa anafahamu lolote kuhusu mahusiano hayo. “Ndiyo,” nilimjibu kwa kumdanganya. “Ila kuwa makini na mapenzi ya facebook wengi wanalia, wengine wanatamani hata kujiua kwasababu ya mapenzi hayohayo ya facebook,” aliniambia Juma maneno ambayo kwa kweli yalinichanganya sana, nilizidi kuwa katika wakati mgumu sana, nilijiuliza maswali mengi ambayo mengi yalikosa majibu. Sikutaka kusikia lolote lile juu ya mtandao huu ambao uliweza kuniachanisha na mke wangu ambaye aliweza kuolewa tena na mwanaume ambaye alimpatia hukuhuku facebook. **** Niliendelea kumsumbua Juliet mpaka pale siku moja alipoweza kunijibu. “Juliet.” “Niambie.” “Mbona upo kimya hivyo?” “Nilikuwa bize.” “Vipi lakini?” “Safi tu.” “Naweza kukuomba kitu?” “Kitu gani?” “Naomba namba zako ili tuwe kunawasiliana kwenye simu kwasababu huku najua sio kila siku tutakuwa tunawasiliana.” “Ok nitumie namba zako,” alinijibu kisha nikamtumia namba zangu na huo mwisho wa chatting zetu. Nilikuwa katika furaha isiyokuwa na kifani, kitendo cha kumuomba Juliet na mba kisha na yeye kuniambia nimtumie namba zangu hakika kiliniweka katika furaha isiyomithilika. Niliamini ule ndiyo ulikuwa mwanzo wa mahusiano yetu ambayo baadae ningeweza kumuoa kabisa, nilikuwa radhi kwa lolote kutoka kwa msichana huyo ambaye nilimpata facebook. Kila siku nilikuwa nikiiangalia simu yangu huku nikitegemea kupokea simu kutoka kwa Juliet lakini hakuna simu wala ujumbe wowote uliyoingia kwenye simu yangu, tukio hilo lilizidi kuniumiza sana. Nilihisi Juliet alikuwa amenidanganya na hivyo asingeweza kunitafuta kabisa. Baada ya kupita wiki mbili ndipo hapo ambapo niliweza kutumiwa ujumbe na namba ngeni. Sikutaka kupoteza muda niliamua kuchat nayo. “Mambo.” “Poa vipi.” “Safi.” “Nani mwenzangu?” “Umenisahau jamani?” “Hujajibu swali lakini?” “Mimi Juliet,” alinijubu. Kwa kweli sikutaka kuamini kama nilikuwa nachat na Juliet, haraka nikaisave namba yake, nilikuwa katika furaha isiyokuwa na kifani. “Juliet jamani ni wewe?” “Ndiyo.” “Mbona sasa umekaa hivyo muda mrefu hata kunitafuta?” “Nilipoteza simu.” “Jamani pole sana sasa namba yangu uliipata wapi tena.” “Siulinitumia facebook, niliingia nikaichukua.” “Nimefurahi sana.” “Usijali.” “Uko wapi?” “Niko nyumbani.” “Hujaenda chuo?” “Hapana.” “Kwanini?” “Nimefukuzwa ada.” “Jamani pole sana.” “Asante sana.” “Kwahiyo utafanyaje?” “Sijui na hapa nilipo nimepanga na mwenye nyumba ananidai kodi yake.” “Kwani huna wazazi?” “Sina walifariki miaka mingi sana iliyopita,” alinijibu Juliet jibu ambalo kiukweli liliniumiza sana. Nilitokea kumpenda sana kwa moyo wangu wote na sikutaka kumuona akiwa katika hali hiyo. Je, nini kitaendelea?

at 12:46 PM

Bagikan ke

0 comments:

Copyright © Braytonofficiallove
Designed by Siyamdezign | Edited By braytonofficiallove
braytonofficiallove | braytonofficiallove | braytonofficiallove
Powered By Blogger
Back to Top