DAWA ZA FANGASI NA JINSI YA KUZITUMIA VIZURI Fangasi ni miongoni mwa vijidudu vya magonjwa vinavyosumbua watu wengi. Magonjwa ya fangasi ni mengi sana na mengine ni hatari sana kiasi cha kuweza kusababisha vifo, hususan kwa watu wenye kinga ndogo ya mwili. Magonjwa yao huwa kwenye ngozi, kwenye damu, kwenye kucha, kichwani, kwenye ubongo na viungo vingine vya mwili. Tatizo kubwa zaidi kwa watu walio wengi ni fangasi wa kwenye ngozi, kucha na nywele. Husababisha mapunye, mashilingi, muwasho, michubuko, vidonda, vipele, harufu mbaya, nywele kutoota vizuri, kucha kukatika au kutoota nk Tatizo la fangasi ni kubwa zaidi kwa watoto, wanawake na wakazi wa maeneo yenye joto na unyevu unyevu. DAWA ZA KUTIBU MAGONJWA YA FANGASI Tuna dawa nyingi za kutibu magonjwa ya fangasi. Dawa hizi zinatofautiana sana kwa uwezo na aina ya fangasi zinazoweza kuwadhibiti vizuri. Kwa hiyo, sio kila aina ya fangasi inaweza kutibiwa kwa dawa yoyote ya fangasi. Dawa za fangasi ni pamoja na 1. Clotrimazole 2. Fluconazole 3. Ketoconazole 4. Griseofulvin 5. Nystatin 6. Itraconazole 7. Econazole 8. Terbinafin 9. Tolnaftate Dawa hizo zipo katika mitindo mbalimbali kama vile vidonge, krimu, losheni, poda, sindano, kimiminika nk. Muhimu : Dawa hizi zinatakiwa kutumika baada ya uchunguzi wa daktari na kushauriwa na daktari na mfamasia. Pia hapa tumeziorodhesha kwa lengo la kukuelimisha tu, kwa hiyo usiende kununua dawa yoyote wala kutumia dawa yoyote kati ya hizo bila kupata ushauri wa daktari. Ni muhimu kutambua kwamba ushauri wa daktari na mfamasia ni muhimu sana kabla ya kununua na kutumia dawa yoyote. Na ukitaka matokeo mazuri hakikisha unatumia dawa vizuri. JINSI YA KUTUMIA VIZURI DAWA ZA FANGASI Fangasi wana tabia ya kuondoka pole pole. Kwa hiyo unaweza ukahisi umepona baada ya kuona muwasho, harufu, majimaji, michubuko, mapunye au mashilingi yamepungua au kupotea. Ukweli ni kwamba inawezekana fangasi bado wapo na ukiwahi kuacha dawa wanajitokeza tena baadae. Fangasi wanaweza kuwepo nje ya mwili na ndani ya mwili. Ni vyema kupata matibabu yanayosaidia kuondoa fangasi sehemu zote ili ukipona upone kabisa na ugonjwa usijirudie au kuwa sugu. Kwa dawa za kupaka na fangasi wa kwenye ngozi hakikisha unaendelea kupaka dawa kwa wiki moja hadi mbili baada ya dalili za fangasi kupotea na kuhisi umepona. Hii inakusaidia wewe kuwamaliza kabisa na kuwazuia wasije wakaibuka tena. Kwa ugonjwa unaohitaji vidonge basi hakikisha unatumia vidonge na unatumia vizuri. Ukitumia ya kupaka peke yake unaweza usipone vizuri, tumia vidonge kama utakavyoshauriwa na daktari na mfamasia wako. Baadhi ya fangasi matibabu yake huchukua muda mrefu. Mifano ni fangasi wanaoathiri kucha na nywele, matibabu yake huweza kuchukua mwezi mmoja au zaidi. Kuwa mvumilivu na maliza dawa zote. Kama una ujauzito ambao ni ngumu kujulikana na daktari au mfamasia wafahamishe kwamba wewe ni mjamzito. Hii itasaidia kukukinga wewe na mtoto dhidi ya dawa ambazo hazifai kwenu. Kama una matatizo ya ini, figo, magonjwa mengine au unatumia dawa zingine ni vyema ukamfahamisha daktari na mfamasia wako pia. Hii ni kwa sababu kuna muingiliano mkubwa sana kati ya dawa za fangasi na magonjwa na dawa zingine kiasi cha kuweza kukuathiri wewe, afya yako na matibabu yako. Tumia dawa zote kama utakavyoshauriwa. Hii ndiyo tiketi ya kupona kwako.

at 7:15 AM

Bagikan ke

Lintaskan

1 comments:

avatar

Mi natumia ya kupaka wakati unanifanyia usafi wa sehem z a sili nikajijeruhi me nikiendelea kupaka kuna máscara ikiingia nilipojichanja

Copyright © 2025 Braytonofficiallove
Designed by Siyamdezign | Edited By braytonofficiallove
braytonofficiallove | braytonofficiallove | braytonofficiallove
Powered By Blogger
Back to Top